Mark 9

1 aIsa akaendelea kuwaambia, “Amin, nawaambia, kuna watu waliosimama hapa ambao hawataonja mauti kabla ya kuuona Ufalme wa Mungu ukija kwa nguvu.”

Isa Ageuka Sura

(Mathayo 17:1-13; Luka 9:28-36)

2 bBaada ya siku sita, Isa akawachukua Petro, Yakobo na Yohana, akawapeleka juu ya mlima mrefu, mahali walipokuwa faraghani. Huko, Isa akageuka sura mbele yao. 3 cMavazi yake yakawa na weupe wa kuzima macho, meupe kuliko ambavyo mtu yeyote duniani angaliweza kuyang’arisha. 4Musa na Ilya wakawatokea, wakawa wanazungumza na Isa.

5 dPetro akamwambia Isa, “Rabi, ni vyema sisi tukae hapa. Turuhusu tujenge vibanda vitatu: kimoja chako, kingine cha Musa na kingine cha Ilya.” 6Petro hakujua aseme nini kwa maana yeye na wenzake walikuwa wameogopa sana.

7 eNdipo pakatokea wingu, likawafunika, nayo sauti kutoka lile wingu ikasema, “Huyu ni Mwanangu mpendwa. Msikieni yeye.”

8Mara walipotazama huku na huku, hawakuona tena mtu mwingine yeyote pamoja nao isipokuwa Isa.

9 fWalipokuwa wakishuka kutoka mlimani, Isa akawakataza wasimwambie mtu yeyote mambo waliyoona, mpaka Mwana wa Adamu atakapokuwa amefufuka kutoka kwa wafu. 10Wakalihifadhi jambo hilo wao wenyewe, lakini wakawa wanajiuliza, “Huku kufufuka kwa wafu maana yake nini?”

11 gWakamuuliza, “Kwa nini walimu wa sheria husema kwamba ni lazima Ilya aje kwanza?”

12 hIsa akawajibu, “Ni kweli, Ilya yuaja kwanza ili kutengeneza mambo yote. Mbona basi imeandikwa kwamba Mwana wa Adamu ni lazima ateseke sana na kudharauliwa? 13 iLakini ninawaambia, Ilya amekwisha kuja, nao wakamtendea walivyopenda, kama ilivyoandikwa kumhusu yeye.”

Mvulana Mwenye Pepo Mchafu Aponywa

(Mathayo 17:14-21; Luka 9:37-43)

14 jWalipowafikia wale wanafunzi wengine, wakawakuta wamezungukwa na umati mkubwa wa watu na baadhi ya walimu wa sheria wakibishana nao. 15Mara wale watu walipomwona Isa, wakastaajabu sana, wakamkimbilia ili kumsalimu.

16Akawauliza wanafunzi wake, “Mnabishana nao kuhusu nini?”

17 kMtu mmoja miongoni mwa ule umati wa watu akajibu, “Mwalimu, nilimleta kwako mwanangu ambaye ana pepo mchafu anayemfanya asiweze kuongea. 18Kila mara huyo pepo mchafu ampagaapo mwanangu, humwangusha chini na kumfanya atokwe povu mdomoni na kusaga meno, kisha mwili wake hukauka. Niliwaomba wanafunzi wako wamtoe huyo pepo mchafu, lakini hawakuweza.”

19Isa akawaambia, “Enyi kizazi kisicho na imani! Nitakuwa pamoja nanyi mpaka lini? Nitawavumilia mpaka lini? Mleteni mvulana kwangu.”

20 lNao wakamleta yule mvulana. Yule pepo mchafu alipomwona Isa, mara akamtia yule mvulana kifafa, akaanguka, akagaagaa chini huku akitokwa na povu kinywani.

21Isa akamuuliza baba yake, “Mwanao amekuwa katika hali hii tangu lini?”

Akamjibu, “Tangu utoto wake.
22Mara kwa mara huyo pepo mchafu amekuwa akimwangusha kwenye moto au kwenye maji ili kumwangamiza. Lakini kama unaweza kufanya jambo lolote, tafadhali tuhurumie utusaidie.”

23 mIsa akamwambia, “Kama ukiweza kuamini, yote yawezekana kwake yeye aaminiye.”

24 nMara baba yake yule mvulana akapiga kelele akisema, “Ninaamini. Nisaidie kutokuamini kwangu!” 25 oIsa alipoona kwamba umati wa watu unakusanyika pamoja mbio, akamkemea yule pepo mchafu, akimwambia, “Wewe pepo bubu na kiziwi, nakuamuru umtoke, wala usimwingie tena!”

26Yule pepo mchafu akiisha kupiga kelele, akamtia kifafa kwa nguvu, na akamtoka. Yule mvulana alikuwa kama maiti, hivyo watu wengi wakasema, “Amekufa.” 27Lakini Isa akamshika mkono, akamwinua, naye akasimama.

28 pBaada ya Isa kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamuuliza wakiwa peke yao, “Mbona sisi hatukuweza kumtoa huyo pepo mchafu?”

29Isa akawajibu, “Hali hii haiwezi kutoka isipokuwa kwa kuomba na kufunga.”

Isa Atabiri Tena Kifo Chake Na Ufufuo

(Mathayo 17:22-23; Luka 9:43-45)

30 qWakaondoka huko, wakapitia Galilaya. Isa hakutaka mtu yeyote afahamu mahali walipo, 31 rkwa maana alikuwa anawafundisha wanafunzi wake. Akawaambia, “Mwana wa Adamu atasalitiwa na kutiwa mikononi mwa watu. Nao watamuua, lakini siku tatu baada ya kuuawa atafufuka.” 32 sLakini wao hawakuelewa kile alimaanisha, nao waliogopa kumuuliza maana yake.

Mabishano Kuhusu Aliye Mkuu Zaidi

(Mathayo 18:1-5; Luka 9:46-48)

33 tBasi wakafika Kapernaumu na baada ya kuingia nyumbani akawauliza, “Mlikuwa mnabishana nini kule njiani?” 34 uLakini hawakumjibu, kwa sababu njiani walikuwa wakibishana kuhusu nani miongoni mwao alikuwa mkuu zaidi ya wote.

35 vAkaketi chini, akawaita wote kumi na wawili, akawaambia: “Kama mtu yeyote akitaka kuwa wa kwanza, hana budi kuwa wa mwisho na mtumishi wa wote.”

36 wKisha akamchukua mtoto mdogo, akamsimamisha katikati yao. Akamkumbatia, akawaambia, 37 x“Mtu yeyote amkaribishaye mmoja wa hawa watoto wadogo kwa Jina langu, anikaribisha mimi. Naye anikaribishaye mimi, amkaribisha Baba yangu aliyenituma.”

Yeyote Asiye Kinyume Nasi Yuko Upande Wetu

(Luka 9:49-50)

38 yYohana akamwambia, “Mwalimu, tumemwona mtu akitoa pepo wachafu kwa jina lako, nasi tukamkataza, kwa sababu yeye si mmoja wetu.”

39 zIsa akasema, “Msimkataze, kwa kuwa hakuna yeyote atendaye miujiza kwa Jina langu ambaye baada ya kitambo kidogo aweza kunena lolote baya dhidi yangu. 40 aaKwa maana yeyote asiye kinyume chetu, yuko upande wetu. 41 abAmin, nawaambia, yeyote awapaye ninyi kikombe cha maji kwa Jina langu kwa sababu ninyi ni mali ya Al-Masihi, hakika hataikosa thawabu yake.”

Kusababisha Kutenda Dhambi

(Mathayo 18:6-9; Luka 17:1-2)

42 ac“Kama mtu yeyote akimsababisha mmojawapo wa wadogo hawa wanaoniamini kutenda dhambi, ingekuwa bora kwake afungiwe jiwe kubwa la kusagia shingoni mwake, na kutoswa baharini. 43 adKama mkono wako ukikusababisha kutenda dhambi, ukate. Ni afadhali kwako kuingia katika uzima ukiwa na mkono mmoja, kuliko kuwa na mikono miwili lakini ukaingia jehanamu, mahali ambako moto hauzimiki. [ 44 aeMahali ambako funza wake hawafi wala moto wake hauzimiki.] 45 afKama mguu wako ukikusababisha kutenda dhambi, ukate. Ni afadhali kwako kuingia katika uzima ukiwa kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili lakini ukaingia jehanamu. [ 46Mahali ambako funza wake hawafi wala moto hauzimiki.] 47 agNalo jicho lako likikusababisha kutenda dhambi, ling’oe. Ni afadhali kwako kuingia katika Ufalme wa Mungu ukiwa na jicho moja, kuliko kuwa na macho mawili lakini ukatupwa jehanamu, 48 ahmahali ambako “ ‘funza wake hawafi,
wala moto wake hauzimiki.’

49 aiKila mmoja atatiwa chumvi kwa moto.

50 aj“Chumvi ni nzuri, lakini ikipoteza ladha yake utaifanyaje ili iweze kukolea tena? Mwe na chumvi ndani yenu, mkaishi kwa amani, kila mmoja na mwenzake.”
Copyright information for SwhKC